Thursday, July 14, 2016

SIMBA KAMILI YAINGIA KAMBINI.

CHINI ya kocha Joseph Omog kikosi cha Simba sasa kitaingia kambini mjini Morogoro kujiimarisha zaidi kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Omog ambaye amemwaga wino wiki iliyopita kukinoa kikosi hicho cha Msimbazi na tayari mapema wiki hii, ameanza mchakamchaka kwa wachezaji wake katika Uwanja wa Bandari Kurasini.
Omog amekuwa akitumia muda mwingi kuwapa mazoezi ya kukimbia uwanja kwa saa tatu pamoja na mazoezi ya viungo, lengo likiwa ni kuwatengenezea stamina na pumzi ili wamudu kucheza dakika 90 uwanjani. “Nimewapa mazoezi ya kuongeza stamina, nguvu na pumzi ili wachezaji wangu wamudu kucheza mpira.


“Nimefikia hatua hii baada ya kuwaona wachezaji wanachoka mapema baada ya kuwapa mazoezi ya kukimbia mbio ndefu na fupi, ninataka timu imudu kucheza dakika zaidi ya 90 katika mechi,” alisema Omog ambaye ameapa msimu ujao Simba inapanda ndege kushiriki michuano ya kimataifa kwani atahakikisha Wekundu hao wa Msimbazi wanamaliza ukame wa mataji.
Alisema ana mifumo mingi mpaka sasa hajajua atumie mfumo upi ambao utaendana na kikosi chake ambacho amekiri hajawafahamu vizuri wachezaji wake na kwamba atakapokaa nao angalau kwa wiki mbili zaidi atajua ni mfumo upi sahihi wa kwenda nao kutokana na aina ya wachezaji wake.
Kikosi hicho kitajichimbia Morogoro kwa muda wa wiki mbili kabla ya kuvuka maji kuweka kambi Zanzibar kwa muda wa wiki mbili ikijiandaa na Ligi Kuu Tanzania bara inayotarajiwa kutimua vumbi Agosti 20 mwaka huu.
Hata hivyo, kabla ya mchakamchaka wa ligi timu hiyo itacheza mchezo wa kirafiki na Gor Mahia kwenye tamasha la Simba Day litakalofanyika Agosti 8 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Rais wa Simba, Evans Aveva amekaririwa akisema wachezaji wote waliosajiliwa na timu hiyo watakwenda kambini Morogoro kwa ajili ya kuanza kujifua wakiwa chini ya Kocha Mkuu mpya Mcameroon Joseph Marius Omog ambaye aliwasili nchini wiki iliyopita na kurithi mikoba ya Muingereza Dylan Kerr, aliyefukuzwa Januari.
Aveva alisema lengo la kuandaa kikosi chao ni kuhakikisha msimu ujao wanafanya vizuri na kuondoa ukame wa vikombe unaokabili klabu hiyo kwa miaka minne mfululizo na kuwapa raha mashabiki na wanachama wao.

No comments:

Post a Comment