Thursday, July 14, 2016

KICHUYA NJIA MOJA SIMBA SC

MAMBO safi baina ya Simba SC na kiungo Shizza Ramadhani Kichuya baada ya kuafikiana kufanya kazi pamoja kwa miaka miwili ijayo.
Winga wa Mtibiwa Sugar ya Morogoro, Shizza amesema amepewa ridhaa na klabu yake, Mtibwa Sugar kufanya mazungumzo na Simba SC.
Kichuya amebakiza mwaka mmoja katika Mkataba wake na Mtibwa, mabingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara mara mbili mfululizo, 1999 na 2000.

 Na akizungumza na BIN ZUBEIRY SPORTS – ONLINE leo, Kichuya amesema kwamba amefanya mazungumzo na uongozi wa Simba SC na kufikia makubaliano ya kuingia Mkataba wa miaka miwili.
“Nimezungumza na Simba na tumefikia makubaliano, lakini kusaini bado, nadhani wakati wowote kuanzia sasa naweza kusaini,”amesema Kichuya ambaye leo alikwenda pia kuzungumza na kocha Mcameroon wa Simba, Joseph Marius Omog mazoezini Chuo cha Polisi Kurasini, Dar es Salaam.
“Asubuhi nilikwenda kwenye mazoezi ya Simba (Kurasini) kwa ajili ya kuzungumza na kocha Omog, nashukuru amenipokea vizuri na amesema yuko tayari kufanya na mimi,”amesema.
Kama atasaini, Kichuya atakuwa mchezaji wa tatu wa Mtibwa kuhamia Simba SC majira haya baada ya Muzamil Yassin na Mohamed ‘Mo’ Ibrahim, wote viungo. 

No comments:

Post a Comment